Searching...
Ijumaa, 22 Novemba 2013

HATARI:WATU 16 WAUAWA KWA WIVU WA KIMAPENZI TANGA

WATU 16 wameuawa mkoani Tanga katika kipindi cha miezi 10 kuanzia Januari hadi Oktoba kutokana na ama wivu wa mapenzi au kukamatwa ugoni. 

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tanga, Costantine Massawe alitoa taarifa hiyo hivi karibuni wakati akiwasilisha taarifa kwa vyombo vya habari kuhusu hali ya ukatili wa kijinsia na watoto mkoani humo kati ya Januari na Oktoba mwaka huu.

Kwa mujibu wa Kamanda, mauaji hayo ni sehemu ya matukio 377 ya ukatili wa kijinsia yaliyojitokeza katika kipindi hicho. Mengine ni makosa 308 ya ubakaji, 46 ya ulawiti, manne ya kutupa watoto na matatu ya wizi wa watoto.

Alisema kati ya matukio hayo, kesi 138 ndizo zinaendelea kusikilizwa zikiwa katika hatua mbalimbali mahakamani. Kesi 166 zinaendelea kupelelezwa na polisi, 57 zilifungwa kutokana na kukosa ushahidi wa kuzipeleka kwa Mwanasheria wa Serikali kwa hatua zaidi za kisheria , 24 zilipata ushindi na kesi sita zilishindwa.

Kamanda ameshauri iwepo miongozo ya kitaifa inayounganisha taasisi muhimu zinazojihusisha na harakati za kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Alisema ukosefu wa miongozo hiyo, unadumaza kasi ya harakati za kupinga vitendo hivyo.

Alisema viashiria vinavyotokana na kuwepo kwa matukio ya aina mbalimbali ya ukatili vinadhihirisha kwamba hali ni mbaya mkoani humo na kwamba jitihada za makusudi zinahitajika kuunganisha nguvu kwa pamoja.

“Takwimu zetu za matukio yaliyoripotiwa kwenye vituo mbalimbali vya Polisi zinaonesha kuwepo kwa makosa haya ambayo ki msingi yanaathiri sana ustawi wa afya ya mwili, akili ya mwathirika pamoja na kuchochea ukiukwaji wa haki za binadamu ndani ya jamii”, alisema na kuongeza.

Kutokana na hali hiyo alisema ipo haja Serikali kujitathmini na kuboresha taratibu za kushughulikia matukio hayo ikiwemo kuunganisha na kuwezesha vyombo vyote vinavyosimamia sheria ili kurahisisha utekelezaji wa majukumu yake katika mchakato mzima wa kupambana na ukatili wa kijinsia.

0 comments:

Chapisha Maoni

 
Back to top!