Searching...
Jumamosi, 6 Julai 2013

RAIS WA VENEZUELA AMPA HIFADHI MMAREKANI SNOWDEN,URUSI YAMTAKA SNOWDEN AONDOKE NCHINI MWAKE,OBAMA AIWEKA KIPORO VENEZUELA

Rais wa Venezuela Nicolas Maduro
RAIS NICOLAS MADURO.
Rais wa Venezuela Nicolas Maduro amesema kuwa ameamua kumpa hifadhi mfanyakazi wa zamani wa shirika la ujasusi la Marekani Edward Snowden, ambaye ametuma maombi kwa nchi kadhaa ili kuepuka kukamatwa na Marekani.
Akizungumza kwa njia ya televisheni wakati wa sherehe za kuadhimisha uhuru wa nchi hiyo, Maduro amesema ameamua kumpa Snowden hifadhi ya kibinadamu katika nchi yake ili aepuke kuandamwa na Marekani. Snowden anaaminika kuwa amejificha katika eneo la abiria la uwanja wa ndege wa kimataifa wa Moscow tangu tarehe 23 mwezi uliopita.
Maduro amesema ameamua kumpa Snowden hifadhi kwa sababu siri aliyofichua imeonesha wazi maovu yanayofanywa na taifa la Marekani.
"Nani ana hatia? huyu kijana mdogo ama serikali ya Marekani ambayo inatoa mabomu na silaha kwa magaidi ambao ni wapinzani nchini Syria dhidi ya watu wa Syria na kiongozi halali rais Bashar Al Assad?" Aliuliza Maduro alipokuwa anawahutubia maafisa wa jeshi waliompigia makofi baada ya tamko lake hilo.
 Edward SnowdenEDWARD SNOWDEN.
Edward Snowden aliye na umri wa miaka 30 anatakikana na Marekani kwa kufichua madai ya mpango wa udokozi wa Marekani dhidi ya washirika wake wa Ulaya. Hata hivyo kwa sasa haijajulikana wazi iwapo Snowden atakubali hifadhi hiyo au ni vipi atakavyopokea habari hiyo ya kupewa hifadhi na Rais wa Venezuela.
 Waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov
 Waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov.
Awali Urusi ilionesha wasiwasi wake juu ya kuwepo kwa mfanyakazi wa zamani wa shirika la ujasusi la Marekani nchini mwake, wakati waziri wake wa mambo ya kigeni Sergei Lavrov aliposema kwamba bado hawajapokea ombi la kutaka hifadhi kutoka kwa Snowden na kwamba ni lazima atafute mahali pa kwenda ili aondoke Urusi. Lavrov amesema kila anapozidi kukaa nchini humo anahatarisha mahusiano mema kati yao na Marekani.
Awali rais wa Nicaragua Daniel Ortega alisema serikali yake iko tayari pia kumpa hifadhi Edward Snowden. Wakati huo huo Marekani imekataa kutoa tamko juu ya hatua ya rais Nicholas Maduro.
Shirika la Wikileaks lilisema Snowden ameendelea kuomba hifadhi kwa mataifa mengine 6 na kuongeza idadi ya nchi alizoomba hifadhi kufikia zaidi ya 20.
HABARI NA DW - SWAHILI.

0 comments:

Chapisha Maoni

 
Back to top!